HABARI MPYA LEO  

MAWAZIRI WALIOACHWA

By Maganga Media - May 5, 2012

Rais Jakaya Kikwete akitangaza Baraza jipya la Mawaziri, Ikulu jana.

RAIS Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko makubwa katika Baraza la Mawaziri kwa kuteua wapya watatu na manaibu 10 huku akiwaacha wanane.

Katika mabadiliko hayo, Rais Kikwete amewapandisha manaibu mawaziri wanne kuwa mawaziri kamili na kuwahamisha wizara mawaziri wanane na manaibu waziri sita, huku mawaziri na manaibu waziri 22 wakibaki katika wizara zao za awali.

Kutokana na mabadiliko hayo, idadi ya mawaziri na manaibu wao sasa imeongezeka kutoka 50 katika baraza la awali hadi 55. Mawaziri kamili wameongezeka kutoka 29 hadi 30 huku manaibu waziri wakiongezeka kutoka 21 hadi 25.

Mawaziri ambao wameng’olewa na wizara walizokuwa wakiziongoza kwenye mabano ni Mustafa Mkulo (Fedha), Dk Hadji Mponda (Afya na Ustawi wa Jamii) William Ngeleja (Nishati na Madini), Dk Cyril Chami (Viwanda na Biashara), Omar Nundu (Uchukuzi) na Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii).

Panga hilo la mabadiliko limewakumba pia Manaibu Waziri wawili, Dk Lucy Nkya (Afya na Ustawi wa Jamii) na Dk Athumani Mfutakamba (Uchukuzi).

Akitangaza baraza hilo Ikulu jana, Rais Kikwete alisema mabadiliko hayo yametokana na mjadala mkali ulioanzia bungeni baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kwamba ametumia fursa hiyo kufanya marekebisho kadhaa ili kuimarisha utendaji wa Serikali.

“Baada ya kuwasilishwa kwa taarifa ile kulikuwa na mjadala mkali bungeni, lakini pia kwenye kikao cha wabunge wa chama na Waziri Mkuu (Mizengo Pinda), alinipa taarifa hiyo na wanasema mawaziri wote waliotajwa waondolewe,” alisema Kikwete na kuongeza:

“Tumekaa kwa pamoja na kumwangalia kila mmoja na tuhuma zake, kwa Kiingereza tunasema ‘case by case’ na tukaona kwamba wawili kati yao tuwahamishie katika wizara nyingine lakini tukatumia fursa hiyo kufanya mabadiliko mengine kwa lengo la kuimarisha utendaji wa Serikali.”

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII