HABARI MPYA LEO  

Utata wa umri wa Lulu kusikilizwa Mei 28 Mahakama kuu

By Maganga Media - May 19, 2012

MAOMBI ya uchunguzi wa umri wa muigizaji wa filamu, Elizabeth Michael maarufu kama Lulu anayekabiliwa na  kesi ya mauaji, yamepangwa kusikilizwa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam  Mei 28, 2012. Lulu anakabiliwa na kesi ya mauaji ya msanii mwenzake, Steven Kanumba, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.Hata hivyo, umri wake halali umezua utata jambo ambalo limewalazimu Mawakili wanaomtetea kuwasilisha maombi mahakamani wakiitaka mahakama ifanye uchunguzi wa umri halali wa msanii huyo.

Maombi yaliwasilishwa Mahakama Kuu na mmoja wa mawakili wake, Peter Kibatala, Mei 17. Habari kutoka mahakamani zinasema kuwa maombi hayo yamepangwa kuanza kusikilizwa Mei 28 na kwamba yamengiwa kusikilizwa na Jaji Dk Fauz Twaib.

Katika maombi namba 46 ya mwaka 2012, mawakili hao wanaomtetea msanii huyo wanaiomba Mahakama Kuu itoe uamuzi kama Mahakama ya Kisutu ina uwezo wa kuamua ufanyike uchunguzi wa umri halali wa msanii huyo. Jopo la mawakili hao maarufu linadai kuwa linaamini kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ambayo kwa sasa ndio bado inayoshughulikia kesi hiyo, ina mamlaka ya kufanya au kuamuru ufanyike uchunguzi wa umri mshtakiwa huyo.

Lakini pia wanaiomba Mahakama Kuu kama itaridhika kuwa Mahakama ya Kisutu haina uwezo huo, basi Mahakama Kuu yenyewe ifanye uchunguzi huo.

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII