HABARI MPYA LEO  

Kauli ya Bavicha kwa SHIBUDA

By Maganga Media - May 17, 2012


Taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa Bavicha, John Heche  imesema baraza hilo limepokea kwa mshtuko taarifa kwamba Shibuda atagombea urais na meneja wake wa kampeni atakuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete na alitoa kauli hiyo kwenye kikao cha Nec ya CCM.

Pia wameshtushwa na kitendo cha Shibuda kusema kuwa hakuna chama kingine chenye uwezo wa kuiongoza nchi kwa sasa na kutoa tamko hilo kwa niaba ya Taasisi inayotathmini Utawala Bora Afrika (APRM).

“Mambo hayo manne ndiyo yametushtua na kutufedhehesha sisi vijana wa Chadema na ndiyo maana, tumelazimika kutoa kauli kuhusiana na suala hili,” alisema Heche.

Heche alisema kamwe Bavicha haitaruhusu mgombea urais wa Chadema kuwa na meneja wa kampeni kutoka CCM akisema kina watu wa kutosha na wenye uwezo wa kufanya kazi hiyo.

“Kamwe hatutaruhusu mgombea urais wa Chadema awe anatangaza nia kwenye vikao vya CCM, kwani hawana mamlaka ya kumteua mgombea wa Chadema na kama Shibuda alikuwa halijui hilo anapaswa kulifahamu kuanzia sasa kuwa vijana wa Chadema hatuchaguliwi mgombea na Nec ya CCM kwani Chadema kuna vikao na taratibu zetu za kuteua wagombea,” alisema Heche.

Alisema kitendo cha Shibuda kusema kuwa hakuna chama kingine chenye uwezo wa kuongoza nchi ni kudhalilisha  vijana wa Chadema na Watanzania wote ambao leo wanakiona chama hicho kama tumaini pekee la kuwakomboa.

“Kwa kauli hii, tunaamini kuwa mamlaka za nidhamu hazitakaa kimya bila kutakiwa maelezo ya kina. Tutaitisha kikao cha Baraza na tutaijadili kauli hii na kuwasilisha mapendekezo yetu kwenye vikao halali vya chama,” alisema na kuongeza:

“Kwa nini atafute urais kwenye chama ambacho anaona hakiwezi kuongoza dola? Anawatania Watanzania? Ni heri akaenda kwenye hicho ambacho anaamini kuwa kinaweza kuongoza dola. Kwani lengo la chama chochote kile ni kuchukua dola na si vinginevyo.”

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII