HABARI MPYA LEO  

Wema na Wolper tayari kwa pambano lao!

By Unknown - Jul 7, 2012


MAHASIMU wawili katika tasnia ya filamu nchini, madada Wema Sepetu na Jacqueline Wolper wanapanda jukwaani leo kuendeleza uhasimu wao, lakini safari hii wakifanya hivyo kwa kuzichapa ngumi 'live'.Kabla ya pambano hilo, wasanii hao wamekuwa wakirushiana maneno ya vijembe vya kejeli, huku kila mmoja akitamba kumshikisha adabu mwenzake.

Pambano hilo la pekee kwa aina yake, litapigwa kwa raundi nne, usiku wa Tamasha la Matumaini kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.Katika kujiandaa na pambano hilo, Wema mshindi wa shindano la Miss Tanzania, 2006 anafundishwa na bondia mkongwe, Rashid Matumla.

Akiongea mwishoni mwa wiki, Wema alisema amejiandaa vizuri kumchakaza mpinzani wake ambaye amesema hatamaliza raundi nne ulingoni."Nimejiandaa kumpiga vilivyo Wolper, sina shaka kwamba hamalizi raundi zote za mchezo," alisema Wema kwa kauli ya kujiamini.

Kocha wa Wema, Matumla alisema jana kuwa amemuandaa vizuri mchezaji wake kumkabili Wolper.
"Nimempa mazoezi mazuri na kumwelekeza sehemu muhimu za kumpiga Wolper ili amkalishe chini kabla ya raundi kumalizika," alisema Matumla.

"Najua Wolper ni mrefu kuliko Wema, lakini hilo siyo tatizo. Kama atashindwa kumchapa usoni, basi atatumia mbinu ya kumchapa makonde tumboni," alitamba Matumla.

Kwa upande wake, Wolper amesema amesikia maneno na vijembe vya kukera dhidi yake toka kwa Wema, na majibu ya kelele hizo atayatoa ulingoni."Wema ameongea sana mpaka inakera, amefanya hivyo kwenye televisheni, radio na magazeti. Mimi siyo mtu wa maneno, napenda vitendo," alisema.

Aliongeza: "Kesho (leo) nitamkata mdomo wake, aache kelele...aache kuchonga. Nina uwezo wa kumpiga Wema nikiwa nimekaa na yeye amesimama."
Wolper alisema hana sababu ya kujiandaa kama anavyofanya Wema kuelekea pambano lao, kwani ana uhakika wa kumtandika.

Baada ya pambano hilo la akinadada, litafuata pambano lingine linalosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa ndondi kati ya Japhet Kaseba na Francis Cheka.Mabondia hao, Alhamisi wiki walirushiana maneno wakati wakiongea na waandishi wa habari, huku kila mmoja akitamba kumgalagaza mwenzake.

Kaseba alisema amejianda vizuri kwa pambano hilo, na kwamba yeye ndiye bingwa wa kweli wa ngumi nchini.
"Nilipopigana na Cheka pambano la kwanza sielewi alishinda vipi, sasa nataka kumwonyesha naweza kumdunda," alisema.

Kwa Upande wa Cheka alisema anapanda jukwaani kuthibitisha ubabe wake kwa Kaseba, ambaye anadai aliokolewa kipigo na mashabiki wake katika pambano lao lililotagulia.

Mbali na burudani hiyo ya ngumi, pia tamasha hilo litapambwa na burudani ya muziki kutoka kwa wasanii mbalimbali akiwamo Diamond, Chameleon kutoka Uganda na wasanii wa nyimbo za Kiroho.

Pia kutakuwa na pambano la soka kati ya timu ya Wabunge mashabiki wa Simba na ile ya mashabiki wa Yanga, huku timu ya Wasanii wa Filamu ikiumizana na timu ya Wasanii wa Muziki wa Kizazi Kipya (Bongo Fleva).

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII