HABARI MPYA LEO  

Mchungaji afukuzwa kanisani kwa uzinzi

By Maganga Media - May 20, 2012

MCHUNGAJI wa Kanisa la Baptisti la Makole katika Manispaa ya Dodoma, John Mwangafike ambaye pia ni Katibu wa Kanisa hilo Tanzania, amefukuzwa katika kazi hiyo ya kumtumikia Mungu kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni kukiuka kwake kwa makusudi maadili ya kichungaji. 

Barua hiyo ambayo ilitiwa saini na Katibu wa Kanisa hilo, Daniel Njonde na Mzee Kiongozi wa Kanisa hilo Simon Marivey Pia ilimtaka Mchungaji huyo kukabidhi mali zote za Kanisa kufikia jana saa nne asubuhi.  “Aidha Kanisa katika kikao cha Jumuiya ndogo ya Dodoma ya Aprili 15, mwaka huu, iliridhia wewe kufukuzwa katika huduma ya kichungaji hapa Kanisa la Kibatisti Makole,” ilisema sehemu ya barua hiyo.

Awali, habari kutoka ndani ya Kanisa hilo zinasema kuwa, Askofu na Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kanisa la Baptisti mkoani hapa, Emmanuel Mwakandulu alisaini barua ya waumini na wazee wa Kanisa hilo, waliotaka Mchungaji huyo asimamishwe kwa tuhuma za kuzaa na waumini, akiwemo msichana wake wa kazi na mwanamke mmoja ambaye ni mke wa mtu ambaye licha ya kuwa na mtoto moja naye, sasa ni mjamzito.

Kusimamishwa kwa mchungaji huyo kuliridhiwa na washirika 47 na wazee wa Kanisa hilo. Kulingana na tuhuma za mchungaji huyo, waumini na viongozi walitaka mchungaji huyo aondolewe kwenye huduma baada ya kukaidi kujiuzulu alipotakiwa kufanya hivyo. Hatua ya kumtimua kiongozi huyo imefanyika kulingana na Imani ya Kibaptisti na Katiba ya Kanisa hilo kifungu Na. 24(9), 27(C) na (F) (10) vinavyozungumzia ukosefu wa maadili.

Aidha, anatajwa kuzaa watoto watatu na mfanyakazi wa ndani ambaye hata hivyo jina lake linahifadhiwa na kuzaa mtoto mmoja mmoja na waumini wake wawili. Inaelezwa katika kikao hicho na wajumbe waliofika kwake, alikanusha kuwa na watoto nje ya ndoa, akisema wanaomwita baba ni `watoto wa kiroho’.

Aidha, inaelezwa Mchungaji huyo alikiri kusafirisha kwa jina la Kanisa chakula kwenda Malawi, akisema waumini wa Kanisa hilo nchini humo wako katika njaa, ingawa hakikuwafikia.

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII