HABARI MPYA LEO  

Wasemayo waandishi juu ya Lulu.

By Maganga Media - Apr 11, 2012

MSANII Elizabeth Michael (Lulu)


Ndugu zangu,

Jana amezikwa Steven Kanumba , kipenzi cha wengi.
 Mauti ya Steven Kanumba yanatukumbusha wanadamu ukweli huu; kuwa maisha yetu hapa duniani ni mafupi sana. Hivyo, lililo jema kwetu wanadamu ni kuishi kwa kutenda yalo mema. Kuwatendea mema hata tunaodhani wametukosea, maana, tutawasaidia kujifunza kutenda mema. Na ni mwanadamu gani asiyekosea?

Na moja ya adhabu kubwa  mwanadamu unaweza kuipata humu  duniani kutoka kwa wanadamu wenzako ni adhabu ya kutengwa na wanadamu wenzako.

Msichana Lulu ameshapata na anaendelea kuipata sasa, adhabu kubwa sana kutoka kwa wanajamii. Adhabu ya kupewa hukumu ya mauaji na kutengwa na wengine. Lulu , ambaye ni mmoja wa waliokuwa karibu na marehemu Kanumba hata katika dakika zake za mwisho maishani, na ambaye alikuwa mpenzi wa Kanumba, hakuweza kushiriki mazishi ya mpenzi wake. Hiyo nayo ni adhabu kubwa kwa Lulu kupewa na wanadamu wenzake.

Yumkini Lulu ana mapungufu yake kama mwanadamu, lakini, kwa sasa hastahili adhabu kali hiyo kutoka kwa wanajamii. Kwa kosa ambalo hakuna aliye na hakika leo kuwa amelitenda. Ndio, Lulu aweza kuwa mwanadamu mwenye mapungufu yake mengine, lakini , hayo yasitufanye wanadamu tuwe na haraka ya kumpa hukumu isiyo ya  haki.  Na kwenye mienendo ya maisha, ni mwanadamu gani asiye na mapungufu?
  
Maana, tangu mara ile ilipofahamika, kuwa msichana Elizabeth ‘ Lulu' Michael alikuwepo kwenye mazingira ya kutokea kwa kifo cha Kanumba, basi, jamii, huku ikisaidiwa na vyombo vya habari, haraka ikapata wa kumnyoshea kidole. Na hukumu ya Lulu kutoka kwa wanajamii walo wengi ikawa imetolewa hapo. Kwamba Lulu ndiye muuaji. Kwa sasa, hukumu hiyo haiwezi ikawa ya haki mpaka pale wenye mamlaka ya kututhibitishia hilo watakapofanya hivyo.

Na  hata kama ugomvi, uliotokana na wivu wa kimapenzi ,  wa  Lulu na mpenzi wake ulipelekea mauti ya Kanumba, bado  maelezo tuliyoyasikia  hayamwonyeshi Lulu kuwa na dhamira ya kutaka kutenda maovu anayohukumiwa na wanajamii kuwa  kayatenda. Hivyo, naye, kama mwanadamu, anastahili msamaha kutoka kwa  wanajamii wengi walo wema.

Katika wakati huu mgumu sana kwa msichana Lulu, vyombo vya habari viwe  mbele katika kumsaidia Lulu kama mwanadamu mwenzetu, badala ya kutumia balaa lililomkuta kama mtaji wa kuandika na kutangaza  udaku wa kuuzia magazeti na kuvutia watazamaji wa runinga na wasikilizaji wa  redio. 

Maana, kwa adhamiriae kutumia magumu yanayomkabili  msichana Lulu kuvuna, basi, hana atakachokivuna zaidi ya kuvuna dhambi.

Badala yake, media isaidie katika kutufanya wanajamii tujitafakari.  Kwa vile, habari za matukio ya mahusiano yasiyo na staha na matendo ya kiuhuni yanayofanywa na baadhi ya wanajamii wakiwemo wasanii,  huwa yanashabikiwa na vyombo vya habari  badala ya vyombo hivyo kushiriki kukemea na kuelimisha jamii. inasikitisha, kuwa katika wakati huu, vyombo hivyo vya habari vyaweza kabisa kuwa  kwenye harakati za kuandaa stori zaidi za ‘ kumning’iniza’ zaidi Lulu ambaye tayari ameshaning’inizwa hadharani.

Ndugu zangu,

Kama wanajamii, na wengine kama wazazi. Lulu anabaki kuwa ni msichana mdogo anayehitaji kusaidiwa katika wakati huu mgumu kwa maisha yake. Yumkini vyombo vya dola vinaweza vimtie au visimtie hatiani. Hivyo,  kumwachia huru Lulu.  

Lakini, bado hukumu ya jamii ikabaki pale pale. Hukumu ya Lulu kutengwa na jamii.  Hiyo ni hukumu mbaya zaidi  inayoweza kuchangia hata kuyafupisha maisha ya msichana huyu mdogo. Jamii haina faida na hukumu kama hiyo.  Ni heri ikamwacha huru aende akapambane na yanayomkabili mbele yake. Ndio, akapambane na  maisha haya magumu ya dunia hii bila kujisikia kutengwa na wanajamii wenzake.

Na naamini, leo  kuna wengi kama mimi,  wenye kufikiri hili, kuwa jamii ya walo wema imsamehe Elizabeth ‘ Lulu’ Michael.

Na hilo ni Neno La Leo.

Maggid Mjengwa
.......................................................................................................................................
Kwanza nawalaumu Watanzania wenzangu wengi wenye uchungu halali kwa kuamua kumrundikia Elizabeth Micheal makosa na kuweka kwenye FAcebook picha zinazooanisha tukio na uwepo wake, na picha ambazo nyingi ni za nusu utupu, kama vile kusema (ukisoma mengi ya maoni ya awali ya Facebook) huyu ndiye shetani. 
Na kwa kweli, kuna ingizo moja la mtu ninayemheshimu sana lilikaribia  kusema hivyo. Nataka niseme kuwa Lulu ni zao la ujenzi- social construction, ambalo limefanywa na sisi wenyewe, na hasa wanaume. 
Namkumbuka mtoto huyu alivyoanza na baadaye wanaume machangu papa walivyoanza kumnyemelea, kumrubuni na kumjengea sura hii aliyo nayo leo.
Hakuna mwanamke anakuwa “Malaya”- kama kweli neno hilo lina maana, bila kuwepo wanaume. Wanaume ndio wafadhili wa hao wanaokuja kuitwa Malaya baaaye. 
Lakini ikifika wakati mwanamke sasa anasema niko tayari kwa kila mmoja- yaani kwa kila mwanaume, tunajitenga, na kusema fulani ni Malaya- lakini sisi ndio tulioanzisha na kumfanya yeye awe hivyo. 
Siamini kama Elizabeth Micheal alijitengeneza, tulimtengeneza, sisi wanaume na nyie wanawake wenzake. Wanawake wangapi wajitokeze waseme kuwa walikuwa karibu naye tangu wakati manyang’au walipoanza kumnyemelea, wakimshauri awe mwangalifu. Nimeona mara nyingi wanawake husifiana kwa kulipa kwa mwili, sura, maumbile, rangi ya ngozi, na kadhalika. 
Lakini wanapokuja kuharibika au kuharibiwa, lawama zinamwendea anayeonekana kuwa ameharibika.  Hatukuwa na sababu ya kumtundika Lulu kama tulivyofanya, tumetumia fikra mgando kudhani wanawake ndio chanzo cha matatizo. 
Ninawafahamu watu kadhaa, ambao wana heshima zao , waliochangia kumfikisha Lulu hapo alipo, lakini kwa sasa wako kimya. Sisi wengine tumechukulia hili la kuulaumu upande mmoja ni kama unyanyasaji wa kijinsia na mwendelezo wa fikra kuwa mwanamke ndio daima chanzo cha kuanguka kwa mwanaume. dhana ya Femme Fatale- yaanii mwanamke mrembo ni hatari ya kifo- ni kushindwa kuona ukweli kuwa mwanamume ndiye aliyejipeleka kwa mwanamke anayedhaniwa hatari. Kwa hiyo kila mtu anahusika na maamuzi yake.
La pili ni kuhusu polisi wetu. Nilidhani kuna umuhimu wa polisi kutoa elimu kwa umma kuhusiana na matukio kama haya. 

Kwanza, kama Kanumba alifariki nyumbani kabla ya dokta wake kufika, na walipofika waliamua kupeleka maiti Muhimbili, ilikuwa ni makosa makubwa.
Nini kilichowafanya wawe na haraka hivyo kabla ya kuita polisi. Polisi walitakiwa kuja nyumbani kuchukua ushahidi wa mapigano kama kweli yalikuwapo. Kuchunguza mwili na kuupiga picha pale pale, na kuchunguza mengi ambayo mtu wa kawaida huwezi kuyatilia mashaka. 
Ilinishangaza kuwa polisi hawakumkamata na dokta wake, nasikia ndugu alikamatwa akaachiwa, na kuwa Lulu alikuwa ameitwa kujieleza na amegoma kuzungumza awali akitaka mwanasheria awepo – ilikuwa sahihi kwani sheria inamruhusu. 
Pili, ilinishangaza kuona kuwa polisi hawajafuatilia maoni kwenye Facebook na kutoa rai kwa waomblezaji kuwa isingekuwa vizuri kwa wananchi kuanza kutoa hukumu dhidi ya mtu fulani au kundi fulani, wakati uchunguzi unaendelea. Imetokea mara nyingi kumsingizia mtu ushiriki katika tuhuma , lakini kwa kutumia ushahidi usio na vielelezo. 
Kuua sio kuwepo karibu na marehemu, hatujui nini kilimfanya marehemu aanguke; kama waligombana hatujui kama ni kweli, na kama ni kweli sijui kama kulikuwa na kusukumana au kutupiana vitu;  polisi walitakiwa kuwa na maelezo juu ya hilo, na uchunguzi wa daktari ungefafanua zaidi. 

Ilikuwa ni ghafula tu waombolezaji wakaanza kumuona Lulu kama aliua, na wengine kiasi cha “kumtemea” mate na kusema tulijua angefikia hapo. Polisi walitakiwa kuingilia kati.
Tangazo moja kwenye redio na TV lingezuia mwenendo huu wa maoni na kusubiri mwisho wa uchunguzi. Sijaona maoni kutoka kwenye magazeti pendwa, naomba allah yasichukue mkondo wa kubuni mambo kwa ajili tu ya kutaka kuuza.

mohamedmusta@gmail.com, 0766959349

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII