HABARI MPYA LEO  

TZS 70 Billion zalipwa kama mishahara hewa ilhali Walimu na Madaktari Wanalia-Zitto

By Mhariri - Aug 15, 2012

Mishahara hewa nchini
Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu makadirio ya mapato na matumizi katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mwaka wa fedha 2012/2013, tulitaja kiasi cha shilingi bilioni 9 ambazo zililipwa kama mishahara kwa watumishi hewa kama ilivyoripotiwa na magazeti ya ‘The Daily News’ na ‘The Guardian’ ya Machi 23, 2011.

Mheshimiwa Spika, ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya tarehe 31 Machi, 2012 inaonesha kwamba kwa mwaka wa fedha 2010/2011 jumla ya shilingi 142,715,827.99 zililipwa kama mishahara kwa wastaafu, watumishi walioacha au kufukuzwa kazi na watumishi wengine ambao hawakustahili. Aidha, ripoti hiyo imeonesha kiasi cha shilingi 1,842,607,565.29 zilizolipwa kama mishahara hewa kwa mwaka wa fedha 2009/2010.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya Waziri wa Fedha kwa kamati ya kudumu ya Bunge ya fedha na uchumi ya tarehe 7 Agosti, 2012 ni kwamba uhakiki wa watumishi  uliofanyika mwezi Januari, 2012 kwenye Halimashauri 133 na kwenye taasisi na wakala za Serikali 154 ulibaini majina 9,949 ya watumishi wasiostahili kuwemo kwenye orodha ya mishahara. Idadi hii ya watumishi hewa ni sawasawa na takribani idadi ya watumishi walioajiriwa katika sekta nzima ya madini kwenye migodi ya dhahabu hapa nchini. Watumishi hewa wanaokaribia 10,000 ni wengi mno na inaonyesha dhahiri namna Serikali isivyo makini katika suala hili ambalo linasababisha upotevu mkubwa wa Fedha za Umma.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Fedha alikiri mbele ya Kamati ya Fedha na Uchumi kwamba mwezi Februari Serikali ililipa shilingi bilioni 5.1 kama mishahara hewa. Hii maana yake ni kwamba Serikali hutumia zaidi ya shilingi bilioni 70 kila mwaka kwa watumishi hewa wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, tunataka fedha hizi wanazolipwa watumishi hewa zitumike kuwalipa walimu na madaktari madai yao kwani ni nyingi na zinatosha sana. Siku zote sababu za Serikali kutotimiza matakwa ya wafanyakazi kwenye sekta ya Afya na Elimu ni kwamba Serikali haina Fedha. Lakini hapa tunashuhudia Shilingi bilioni 70 kila mwaka zikiteketea kulipa watumishi hewa ambao hawapo, hawafanyi kazi na hivyo kufaidisha mtandao wa kifisadi ambao kwa vyovyote vile unaanzia Wizara ya Fedha na Wizara ya Utumishi. Serikali inakosa vipi fedha za kulipa madai ya Walimu na inapata za kulipa watumishi hewa? Serikali inakosa vipi fedha za kulipa Madaktari na Manesi lakini inapata shilingi bilioni 70 kila mwaka kulipa watumishi hewa?

Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inataka mradi huu wa watumishi hewa wenye mauzo (turnover) ya shilingi 70 bilioni kwa mwaka uvunjwevunjwe ili kupata fedha za kulipa Walimu na Madaktari. Waziri wa Fedha asambaratishe mtandao huu mwovu ambao sasa umeota mizizi kwenye Taasisi za Serikali. Vile vile Waziri agawe kwa Wabunge taarifa ya uhakiki wa wafanyakazi wa Serikali na pia hatua ambazo Serikali imechukua dhidi ya vinara wa mtandao wa watumishi hewa Serikalini.
SOURCE: http://zittokabwe.wordpress.com/

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII