HABARI MPYA LEO  

Bi harusi afa, Bwana harusi apona!

By Unknown - Jul 21, 2012

Stori:Mwandishi Wetu

HUKU majonzi yakiwa bado yametawala miongoni mwa Watanzania kufuatia vifo vya watu waliokuwa ndani ya meli ya MV Skagit ambayo ilipinduka na kuzama Julai 18, 2012 karibu na Kisiwa cha Chumbe, Zanzibar mambo mengi yameibuka.

Nje ya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik siku ya Jumatano (juzi) ambako serikali ilikuwa ikitoa ripoti ya maendeleo ya uokoaji, baadhi ya watu walikuwa katika hali ya majonzi kufuatia ndugu zao kutojulikanna walipo.

Hamis, aliyedai ni mfanyakazi wa Kampuni ya Azam ya tajiri Said Salim Bakheressa alisema mdogo wake, Khalfan na mchumba wake, Zaina Ally walikuwa ndani ya meli hiyo kwenda Zanzibar kufunga ndoa Alhamisi (juzi) kama maandalizi ya kuukaribisha Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, lakini mpaka siku hiyo mdogo wake aliokolewa, ila Zaina hajulikani alipo.

Hamis alisema: “Naamini shemeji yangu amefariki dunia, kwani katika watu wote waliokolewa hayupo, maskini mdogo wangu (Khalfan), alikuwa akafunge ndoa ili wakati wa swaumu mkewe awe halali kumpikia chakula.”

Akaongeza: “mbaya zaidi, mpaka muda huu (saa saba mchana Alhamisi) serikali imetangaza kupatikana kwa miili mingine nane, lakini pia shemeji yangu hayupo.”

Hamis aliongeza kuwa ndoa hiyo ilikuwa ifungwe jijini Dar wiki iliyopita, lakini wazazi wa Zaina ambao wote wanafanya kazi serikalini Zanzibar waliomba ikafungwe visiwani humo.

MENGINE YA KUSHANGAZA
Mtu mwingine ambaye hakutaja jina lake, alisema siku ya tukio, yeye alimsindikiza mdogo wake mpaka bandarini, akiwa anapanda meli hiyo, yeye akaondoka kuendelea na shughuli zake.

“Sasa niliposikia meli imezama, nikampigia simu, hakupatikana, nikajua tayari. Nilituma habari kwa ndugu mbalimbali tayari kwa maandalizi ya msiba.

“Lakini ilipofika saa kumi na mbili jioni akanipigia simu akiniuliza kama nimesikia kuna meli imezama. Nilishtuka, nikahisi naongea na mzimu, nilipomuuliza ameponaje akasema alighairi akapanda meli nyingine, alipofika Zanzibar simu yake ikazima kwa sababu ya kuishiwa chaji.”

Naye mzee Fasha Abduel, mkazi wa Magomeni, jijini Dar, alisema siku hiyo ya tukio, asubuhi alimpeleka bandarini mtoto wa mdogo wake aitwaye Shaban na alimkatia tiketi kwenye meli hiyo, lakini kijana huyo alikuwa hataki kwenda Zanzibar ambako ndiko aliko baba yake mzazi.

“Kumbe nilipoondoka kwenda kazini kwangu (Manispaa ya Temeke) na yeye akageuza kurudi nyumbani. Ajali ilipotokea nilishtuka sana, nikampigia simu mdogo wangu kule Zanzibar, akaanza kilio. Nilipompigia mke wangu kumjulisha, akasema mbona Shaban alirudi muda uleule wa asubuhi na amejaa tele nyumbani,” alisema mzee huyo.

Mzee Hassan, mkazi wa Kariakoo, jijini Dar, yeye alikuwa akipeleka magunia matupu Zanzibar, lakini asubuhi wakati akijiandaa, mwanaye wa kiume, Ally anayesoma Shule ya Msingi Makurumla, Dar aliugua ghafla, hivyo ikabidi yeye akatume magunia hayo kwenye meli hiyo na kumtaarifu mtu wa kuyapokea Bandari ya Malindi, Zanzibar ikawa salama yake.

HABARI HII NI KWA HISANI YA GLOBAL PUBLISHERS


JIUNGE NA CREW YA WAJANJA WA VODACOM

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII