HABARI MPYA LEO  

Wasifu wa Bingu wa Mutharika

By Maganga Media - Apr 6, 2012

Bingu wa Mutharika, aliyekuwa Rais wa Malawi amefariki Dunia tar 06.04.2012
Bingu wa Mutharika amekuwa na ndoto ya kutawala Malawi tangu wakati wa utawala wa mabavu wa Hastings Kamuzu Banda kuanza kusambaratika mnamo mwaka 1993. Ndoto hiyo ilitimia kwanza mwezi wa Mei mwaka 2004 na miaka mitano baadae akapata muhula wa pili kwa ushindi wa kishindo.
Lakini mihula yote miwili ilikumbwa na migogoro na wakosoaji wake walimshinikiza Bwana Mutharika ajiuzulu wakisema kwamba ameifisidi nchi hiyo. Ameshtumiwa kwa kukandamiza uhuru wa demokrasia na pia kuvuruga uchumi.

Mnamo mwaka 2011, wakati wananchi wakikabiliwa na mfumuko wa bei na ukosefu wa mafuta, ghadhabu zao ziliibuka mitaani na nchi kukabiliwa na ghasia mbaya kuwahi kutokea katika historia yake. Takriban watu 19 waliuwawa na polisi waliowafyatulia risasi.

Tuhuma na migogoro

Aprili 2011, Mutharika alimfukuza balozi wa Uingereza nchini Malawi baada ya barua pepe ya kidiplomasia kufichuliwa ambapo balozi huyo alimshtumu Bwana Mutharika kwa kuzidi kutumia mabavu katika utawala wake na kutovumilia wakosoaji wake. Baadaye Uingereza ambayo ndio wafadhili wakubwa wa misaada kwa Malawi ilisema inasitisha misaada yake yote na kuishtumu serikali kwa kufisidi uchumi na kukiuka hali za binadamu.

Na mapema mwaka huu aliwaambia wahisani kutoka ng'ambo "watokomee jehanamu" na kuwashtumu kwa kupika njama pamoja na vikundi vya nchini Malawi za kuipindua serikali yake. Hali kadhalika kumekuwepo na sakata nyingi za kisiasa wakati wa utawala wa Mutharika.

Mnamo mwaka 2010, alimfukuza naibu wake Joyce Banda kutoka chama tawala cha -Democratic Progressive Party lakini hakuweza kumuondoa kutoka wadhifa wa Makamo Rais kwa kuwa alichaguliwa kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi wa 2009.

Chanzo cha ugomvi kati yao ni mipango ya Bwana Mutharika kumteua ndugu yake Peter, ambae ni waziri wa mambo ya nje ,akubaliwe kua mgombea urais wa chama cha DPP katika uchaguzi wa mwaka 2014.

Banda aliunda chama chake mwenyewe cha - People's Party - na chini ya katiba yeye ndiye anayepaswa kushikilia hatamu za uongozi .

Nchi wahisani zilionya mnamo mwaka 2005 kwamba mchuano wa kuwania madaraka kati ya Mutharika na Rais aliyemtangulia Bakili Muluzi umeitenga serikali na matatizo muhimu mkiwemo ukosefu wa chakula.

Bw Mutharika alianza kuhudumu katika mashirika ya uma katika enzi za Rais muasisi Hastings Banda, aliposhika madaraka 1964. Mutharika alikua raia wa Malawi wa kwanza kushikilia wadhifa katika utumishi wa serikali ambapo siku hizo ukidhibitiwa zaidi na Waingereza.

Lakini katika kile kilichoelezwa kua "mgogoro wa baraza la mawaziri "mwaka huo huo,alitoroka Malawi kwa kuhofia kwamba Banda angemhusisha na mawaziri walioasi.

Alienda nga'mbo kwa masomo nchini Zambia, India na Marekani ambako hatimae alijipatia shahada ya uzamifu katika maswala ya uchumi. Baadae alitumikia mashirika kadhaa ya kimataifa ikiwemo Benki ya Dunia.

Wakati wa muhula wake wa kwanza,Bw Mutharika alisifiwa sana kwa kuwasaidia wakulima masikini wa nchi hio kwa kuwapatia ruzuku za pembejeo. Lakini wahisani wakaanza kuionya serikali kwamba isingeweza kumudu mpango mkubwa kama huo na uhusiano wao ukaanza kuharibika.

Kubadili majina

Rais Bingu wa Mutharika
Alipozaliwa alipewa jina Ryson Webster Thom katika wilaya ya iliyokuza chai kwa wingi ya Thyolo mnamo mwaka 1934, lakini mwana huyu wa mwalimu mkuu wa shule alijipa jina la Kiafrika la Bingu Mutharika wakati bara la Afrika lilipokumbwa na vuguvugu la ukombozi wa Afrika katika miaka ya 1960.

Baadae aliongeza "wa" ili kuwababaisha makachero wa Bwana Banda waliokuwa wakiwasaka wapinzani wake duniani kote.

Mnamo mwaka 1992 alikua mwanachama mwaanzilishi wa kikundi cha siri cha wanaharakati wa kisiasa cha United Democratic Front (UDF). Kikundi hicho baadae kikageuzwa kuwa chama cha kisiasa ambacho hatimae kilitawala Malawi kwa kipindi cha miaka 10 baada ya uchaguzi wa kwanza chini ya mfumo wa vyama vingi.

Aliwania urais kwa mara ya kwanza katika uchaguzi wa 1999 lakini aliibuka wa mwisho miongoni mwa wagombea watano.nAlitoweka kwa muda lakini akaibuka tena baadae na bila kutarajiwa akachaguliwa kua mgombea urais wa chama cha UDF baada ya Rais Muluzi kushindwa katika juhudi zake za kugombea muhula wa tatu.

Bw Muluzi, ambae alijigamba kua "mhandisi wa siasa" alimnadi Bw Mutharika kwa wananchi wa Malawi kua ni "mhandisi wa uchumi" na kumnadi nchini kote.Hata hivyo lilikua jambo la kushangaza sana kwamba walikorofishana mara tu baada ya uchaguzi.

Mutharika akajitoa kutoka UDF na kuunda chama chake cha Democratic Progressive Party.

Bw Mutharika aliwalaumu washirika wake wa zamani wa UDF kwa mpasuko huo akisema walichukizwa na juhudi zake za kupambana na rushwa. Chama cha UDF kimekua mstari wa mbele kumfungulia mashtaka Bw Mutharika kua alitumia fedha za serikali kuunda chama chake na tuhuma nyingine za kukiuka katiba. Alikanusha madai hayo akisema yamechochewa na siasa.

Mutharika, alikua ni muumini mkubwa wa kikatoliki aliezaa watoto wanne na mkewe, Ethel, aliefariki 2007. Mwaka 2010, alimuoa aliyekua waziri wa utalii Callista Chapola-Chimombo.

Kutoka BBC

Follow Maganga Media on Twitter, Feel free to like and comment Facebook. Stay updated via RSS

ANDIKA MAONI YAKO KUHUSU HABARI HII